Kwa mujibu wa Ripoti ya Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA- Vyanzo rasmi vya Israel vimeripoti vifo vya Wazayuni 4 na majeruhi 200 baada ya wimbi la mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani (drones) kutoka Iran. Operesheni hii ilifanywa kama jibu la mashambulizi makubwa ya anga ya Israel dhidi ya ardhi ya Iran alfajiri ya Ijumaa.
Kulingana na mitandao ya habari ya Kizayuni "Kan" na "Channel 12," Iran imetumia takriban makombora 200 ya balistiki kuelekea malengo mbalimbali katika maeneo ya kati na kaskazini mwa Israel tangu usiku wa jana. Baadhi ya makombora hayo yaliwalenga miji ya Rishon Lezion na Ramat Gan karibu na Tel Aviv.
Mamlaka za Israel zimeripoti kuwa watu watatu waliuawa Rishon Lezion na mtu mmoja Ramat Gan. Wakati huo huo, Channel 13 ya Israel imeripoti uharibifu mkubwa katika mji mkuu wa Tel Aviv, ambapo majengo na magari mengi yamepata madhara.
Gazeti la Haaretz linaripoti majengo 9 yameharibika kabisa Ramat Gan, na wakazi 300 wa eneo hilo wamehamishwa. Pia, jengo la ghorofa 32 mjini Tel Aviv limepata uharibifu mkubwa.
Kamanda wa polisi wa Tel Aviv alielezea mashambulizi haya kama tukio kubwa lililolenga maeneo kadhaa. Alisema baadhi ya makombora yaliweza kuharibu ghorofa nzima za majengo, na timu za msaada zinaendelea kuhamisha watu waliokuwa wamekwama katika mabwawa ya dharura.
Mzozo unaendelea na vitisho vya kuongezeka kwa mashambulizi
Jeshi la Israel limetangaza kuwa mashambulizi ya Iran yameendelea hadi asubuhi ya leo na vikosi vya ulinzi vimeweza kuzuia ndege zisizo na rubani katika maeneo ya Bahari ya Kufa, Jabal al-Khalil, Wadi Araba na bandari ya Eilat.
Kwa upande mwingine, ndani ya Israel, ripoti zinasema kombora limelenga kituo cha kimkakati Tel Aviv na kusababisha kukatika kwa umeme sehemu za katikati mwa Israel. Hospitali ya Wolfson mjini Tel Aviv imeripoti kupokea majeruhi 21, mmoja akiwa katika hali mbaya.
Operesheni “Wa'de Saadiq 3”
Jeshi la Mapinduzi la Kiislamu la Iran limetangaza kuwa operesheni inayoitwa “Wa'de Saadiq 3” ilifanyika kama majibu ya mashambulizi ya anga ya Israel, na ilitumia makombora mahiri yenye teknolojia ya hali ya juu na mifumo ya kijeshi ya kisasa.
Msemaji wa jeshi la Iran amewaonya kuwa mashambulizi yajayo yatahusisha kurusha makombora elfu mbili kwa wakati mmoja, ambayo ni mara 20 zaidi ya mashambulizi ya sasa.
Iran pia imeripoti kuangamiza ndege zisizo na rubani za kijasusi za Israel katika maeneo kama Selmas, Urmia, Ardabil na Mariwan, na kusema jumla ya drones 5 zimerushwa chini.
Chanzo cha kijeshi cha Iran kimesema: “Vita vitaongezeka siku zijazo, na maeneo yote yaliyokaliwa na Marekani pamoja na vituo vyake katika eneo hili viko hatarini. Wavamizi watatozwa gharama kubwa.”
Baada ya mashambulizi haya, maonyo ya hatari yalisikika katika maeneo mengi ikiwemo Yerusalemu, Tel Aviv na miji ya Wazayuni katika ukanda wa magharibi wa Mto Jordan, na utawala wa Kizayuni ukaingia katika hali ya tahadhari kubwa kabisa.
Afisa mmoja wa ngazi ya juu wa Iran aliiambia Reuters:
"Hakuna sehemu salama ndani ya Israel, na hii ni mwanzo tu wa majibu yetu."
Your Comment